Comments

Zitto Kabwe Hatarini Kukikosa kiti cha ubunge:Hii ni baada ya CHADEMA kumvua rasmi uanachama

Chama  cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimetangaza rasmi kumvua uanachama Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe, kwa madai ya
kukiuka katiba ya chama hicho kutokana na kukishtaki mahakamani.
 
Uamuzi wa Chadema umechukuliwa baada ya Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Saalam jana kutengua pingamizi lililowekwa na Zitto katika kesi aliyoifungua mahakamani kuzuia kujadiliwa na Kamati Kuu ya Chadema hadi kesi yake ya msingi itakapomalizika.
 
Mwanasheria Mkuu wa Chadema, Tundu Lissu, akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam, alisema Zitto alikiuka   katiba ya chama hicho kifungu cha 8(a)(X) ya kukipeleka mahakamani.
 
Alisema  matatizo ya wanachama yatashughulikiwa kwa mujibu wa maadili na nidhamu yaliyopo ndani ya katiba ya chama hicho.
 
Lissu alisema pamoja na katiba ya chama kueleza utaratibu, lakini katika hali ya kushangaza, Zitto alikwenda mahakamani kukishtaki chama huku akifahamu wazi kuwa endapo atashindwa atakuwa amefukuzwa uanachama.
 
“Kwa mujibu wa Katiba ya Chadema kifungu cha 8(a)(X), mwanachama yeyote anapofungua kesi mahakamani dhidi ya chama, endapo atashindwa atakuwa amejiondoa uanachama,” alisema Lissu.
 
 “Zitto `ali-risk' mwenyewe kukipeleka chama mahakamani huku akifahamu wazi kuwa  endapo akishindwa atakuwa siyo mwanachama tena, alishauriwa vibaya ili akiharibu chama badala yake kimezidi kuimarika kuliko kilivyokuwa awali, matokeo yake tumemshinda na hicho kifo kilichotabiriwa hatujakiona, tumezidi kuwa imara kuliko ilivyokuwa awali,” alisema.
 
Aliongeza kuwa mahusiano kati ya chama na Zitto yalivunjika siku nyingi na walichokuwa wanasubiri ni uamuzi wa mahakama tu.
 
Sisi hatuwezi kukubali kuwa na akina Yuda Eskarioti ndani ya chama chetu, taratibu zinazotakiwa kufanywa na chama hivi sasa ni kuiandikia barua Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec) ili iwasiliane na mamlaka husika kwa ajili ya hatua zaidi,” alisema.
 
Alisema hatua nyingine itakayofuata mahakama itajulishwa kwamba Zitto si mwanachama tena kulingana na katiba ya chama hicho.
 
Lissu alisema baada ya mahakama kutoa uamuzi wa kesi aliyoifunga Zitto, Kamati Kuu ya Chadema haina haja ya kukaa na kujadili tena suala lake, isipokuwa Mahakama itatake notisi kuwa siyo mwanachama tena.
 
ZITTO ANENA
Kutokana na hali hiyo, Zitto jana alinukuliwa katika mitandao ya kijamii (facebook na Twitter) akisema hajui lolote kuhusiana na uamuzi uliofikiwa na mahakama na hakuwa na wito kuitwa mahakamani jana. 
 
Alisema Jaji aliyekuwa akisikiliza kesi hiyo amehamishiwa mkoani Tabora na hivyo hakuwa na taarifa ya jaji mpya aliyepangiwa kuendesha kesi hiyo.
 
Kwa kesi ya Tegeta Escrow ilivyokuwa ingeshangaza waathirika kukaa bila kunivuruga, bahati mbaya sana sivurugiki ni kazi tu, mwanasheria wangu atatoa taarifa,” aliandika Zitto katika mitandao ya kijamii.
 
HUKUMU YA MAHAKAMA
Kabla ya Chadema kutangaza kumvua uachama Zitto, Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, ilitangaza kutupilia mbali na kuifuta kesi iliyofunguliwa na Zitto dhidi ya Kamati Kuu ya Chadema, baada ya kukubali pingamizi zilizowasilishwa na chama hicho.
 
Uamuzi huo ulitolewa jana na Jaji Richard Mziray, baada ya kupitia hoja za pande zote mbili kuhusu pingamizi za Chadema.
 
Ilipofika saa 3:20 asubuhi, Jaji Mziray alisoma uamuzi huo mbele ya wanaodaiwa kuwa wanachama wa Chadema huku upande wa Zitto ukiwa hauna mwakilishi na alikuwapo wakili wa utetezi, Peter Kibatala.
 
Alisema baada ya kupitia hoja za pande zote mbili, mahakama imeona Zitto alikosea kuifungua kesi hiyo katika Masijala Kuu ya Mahakama Kuu badala ya Masijala ya Kanda ya Dar es Salaam ya mahakama hiyo.
 
Pia, Zitto hakuonyesha kwa sababu gani alifungua kesi hiyo ya madai Mahakama Kuu badala ya Mahakama ya Hakimu Mkazi kama Sheria ya Mwenendo wa Kesi za Madai.
 
Chadema kupitia mawakili wake, iliwasilisha kwa njia ya maandishi pingamizi dhidi ya kesi hiyo iliyofunguliwa na Zitto.
 
Katika pingamizi ya kwanza, Chadema ilidai kwamba haikuwa sahihi kesi kufunguliwa Mahakama Kuu kwa sababu ilipaswa kufunguliwa Mahakama ya Wilaya/ Hakimu Mkazi kwa mujibu wa Sheria ya Mwenendo wa Kesi za madai.
 
Pingamizi jingine ni kwamba kesi hiyo ilikosewa kufunguliwa Mahakama Kuu, Masijala Kuu badala ya Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam.
 
Jaji alikubali pingamizi hizo kwamba ziko sahihi na kuitupilia mbali kesi hiyo.
 
“Mahakama inaamuru Zitto kukilipa Chadema gharama zote za kesi hii,” alisema Jaji Mziray.
 
Januari 2, mwaka 2014, Mahakama Kuu iliyoketi chini ya Jaji John Utamwa, ilitoa zuio la muda kwa Kamati Kuu ya Chadema kujadili uanachama wa Zitto katika kikao cha chake kilichofanyika  Januari 3, mwaka jana.
 
Hata hivyo, Januari 3, mwaka 2014, mahakama hiyo ilisikiliza hoja za mawakili wa pande zote mbili kuhusu maombi hayo mbele ya Jaji John Utamwa.
 
Januari 7, mwaka 2014, mahakama hiyo pia ilitoa amri kwamba Zitto asijadiliwe uanachama wake hadi kesi ya msingi itakaposikilizwa na kutolewa maamuzi. 
 
Katika kesi hiyo, Zitto alikuwa anatetewa na wakili, Albert Msando, huku Chadema ikiwakilishwa na mawakili Lissu na Peter Kibatala.
 
Katika kesi ya msingi, Zitto alifungua kesi dhidi ya Baraza la Wadhamini la chama hicho na Katibu Mkuu, Willibrod Slaa, akiiomba mahakama itoe zuio la muda la Kamati Kuu kujadili suala la uanachama wake hadi kesi ya msingi itakaposikilizwa na kutolewa maamuzi na mahakama hiyo.
 
Katika maombi yake, Zitto aliiomba mahakama kuiamuru Kamati Kuu ya Chadema (CC) na chombo chochote kisijadili uanachama wake hadi rufaa yake itakaposikilizwa katika Baraza Kuu la Chama.
 
Kadhalika, aliiomba mahakama imwamuru, Dk. Slaa kumkabidhi  nakala za taarifa na mwenendo mzima wa vikao vilivyomvua uongozi ili akate rufaa katika ngazi ya juu ya chama hicho.
 
MSOMI AZUNGUMZA 
Mhadhiri Mwandamizi wa Sayansi ya Siasa na Utawala wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Dk. Benson Bana, akizungumzia hukumu hiyo alisema Zitto ni mwanasiasa ambaye bila shaka anacheza na mifumo.
 
Alisema Zitto anaweza akakata rufani ngazi ya mahakama inayofuata, ili kipindi chake cha ubunge kimalizike aweze kupata mafao yake.
 
Dk.  Bana alisema anasikia kuna chama kinamnyemelea, hali inayoweza kumfanya aende katika chama hicho, na kwamba wamesoma kuwa atafanya uamuzi huo wakati wowote mwezi huu.
 
“Ni kijana bado, anazo njia nyingi za kuendelea kufanya siasa, kwa kuwa taifa bado linamhitaji kama kijana mfanyasiasa za vyama vya siasa,” alisema.
 
KILICHOMPONZA ZITTO
Zitto alisimamishwa Unaibu Katibu Mkuu wa Chadema na Naibu Kiongozi Mkuu wa Upinzani Bungeni na Kamati Kuu ya Chadema sambamba na Profesa Kitila Mkumbo, aliyesimamishwa ujumbe wa Kamati Kuu pamoja na Samson Mwigamba, aliyesimamishwa Uenyekiti wa chama hicho Mkoa wa Arusha.
 

Wote walituhumiwa kuandaa waraka wa siri wa mabadiliko uliokuwa unadaiwa kutaka kufanya mapinduzi ya viongozi wakuu. 
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

New Hope Company. Powered by Blogger.

Facebook

Wazo Hai

Search This Blog

Blog Archive

Flickr

Social Share

Featured
Featured

Labels

Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

TANGAZA NASI HAPA

East Africa Radio Live Here

Tags

Fashion

Sponsor

Videos